Saturday, March 21, 2015


Niger yaomba msaada wa kuwahudumia wakimbizi



Viongozi wa Niger wametangaza kuwa, nchi hiyo haina uwezo wa kuwahudumia wakimbizi wanaoingia nchini humo wakitokea katika nchi jirani ya Nigeria. Maafisa wa serikali ya Niger wanasema, wimbi la wakimbizi wanaoingia nchini humo limekuwa kubwa mno kiasi cha kushindwa nchi hiyo kukabiliana nalo. Taarifa zaidi zinasema kuwa, Niger imeiomba jamii ya kimataifa iisaidie ili iweze kuwahudumia wakimbizi hao. Taarifa ya serikali ya Niger imebainisha kwamba, inaitaka jamii ya kimataifa iisaidie chakula, ujenzi wa makazi ya muda na huduma za kitiba na kiafya. Wimbi la wakimbizi wanaoingia nchini Niger limeifanya nchi hiyo ikabiliwe na hali mbaya zaidi hasa kwa kuzingatia kwamba, nchi hiyo yenyewe ni miongoni mwa nchi masikini zaidi duniani na imekuwa ikitaabika kwa ukame na majanga mbalimbali ya kimaumbile. Wakimbizi hao wamekuwa wakiingia Niger kutokea Nigeria wanakokimbia mashambulio ya kundi la kigaidi la Boko Haram. Mashambulio ya kundi la Boko Haram la Nigeria yamepanuka zaidi na kutishia usalama wa raia katika nchi jirani na nchi hiyo ikiwemo Niger, Cameroon na hata Chad. Nchi jirani na Nigeria tayari zimeunda kikosi cha pamoja cha kukabiliana na wanamgambo wa Boko Haram.
 

No comments:

Post a Comment