Saturday, April 4, 2015

WAZAZI WASHINDWA KUDHIBITI MATUMIZI YA MITANDAO KWA WATOTO WAO.

 

Hamjambo nduguzangu, na karibuni kujiunga nami katika makala hii ambayo huangazia taathira za teknolojia mpya za mawasiliano na habari hasa intaneti katika mtindo wa maisha ya mwanadamu. Katika muundo wa vyombo vya habari duniani bado tunashuhudia uwajibikaji. Hii ndio sababu kuna televisheni au mashirika ya filamu ambayo hutangaza wazi kuwa baadhi ya filamu au vipindi vitazamwe tu na watu wa umri maalumu. Lakini baada ya kuibuka intaneti na kuenea idadi ya watumizi wake miongoni mwa watu wote katika jamii kumejitokeza hatari kubwa. Tunakumbusha hapa kuwa kama ambavyo intaneti ina faida kubwa sana pia inaweza kuwa chanzo cha matatizo na hatari kubwa haswa kwa watoto.
Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, idadi kubwa ya wazazi hawadhibiti namna watoto wao wanaovyotumia intaneti na wala hawalipi uzito suala hilo. Hata baadhi ya wazazi hawajui namna ya kutumia intaneti ili waweze kudhibiti na kusimamia utumizi wake miongoni mwa watoto wao. Kwa hivyo kuna haja kubwa kwa wazazi kujifunza matumizi ya intaneti ili waweze kudhibiti na kusimamia namna watoto wao wanavyotumia teknolojia hii mpya na ya kisasa. Kutokana na kuwa kizazi cha teknolojia hubadilika sambamba na kubadilika kizazi cha wanaadamu, kwa ujumla wale wenye umri wa juu huwa wavivu au wasio kuwa na hamu ya kukumbatia kizazi kipya cha teknolojia. Natija ya awali ya mgongano huu ni kuibuka ufa mkubwa baina ya vizazi sambamba na kutofautiana kuhusu namna ya kutumia teknolojia ya mawasiliano. Hatimaye huwa tunashuhudia mtoto akichukua mahala pa mzazi au mwanafunzi mahala pa mwalimu katika kutoa mafunzo kuhusu utumizi wa teknolojia mpya. Kutokana na kuwa wazazi wengi wana ujuzi wa chini katika masuala ya teknolojia ikilinganishwa na watoto wao, wakati mwinginine hushuhudiwa kutokuwepo na heshima ya kutosha katika uhusiano wa mzazi na mtoto. Kwa msingi huo kuna haja ya watoto kuzingatia maadili ya kijamii na kuwapa wazazi heshima wanayostahiki ili msingi wa familia uweze kudumishwa.
Aghalabu ya watoto hasa wenye umri wa chini huitazama intaneti kama chombo cha kujifurahisha na kuchezea. Kwa hivyo watoto wanakabiliwa na hatari kubwa zaidi kwani hawajui ni jambo gani wanalotaka na kulitafuta. Moja ya nuksani kubwa ya intaneti ni kuwa inatoa maudhui mbaya na nzuri papo hapo.
Kutokana na kuenea intaneti ndani ya nyumba ima kupitia kompyuta za kawaida au simu za mkononi tumeshuhudia namna malezi ya kiintaneti yanavyochukua nafasi ya malezi ya kifamilia. Tunashuhudia kustawi kwa kasi teknolojia ya habari na mawasiliano na hivyo mtoto wa sasa anaweza kutumia intaneti kujua takribani kila kitu pasina kuwepo mipaka. Hivi sasa fmailia nyingi hasa katika nchi zilizostawi haziwezi kuwazuia watoto wao kutumia teknolojia za kisasa kama vile intaneti na hivyo ile mipaka ya kuta nne za nyumba haiko tena. Kuna natija mbili kuhusu utumizi wa intaneti miongoni mwa watoto, awali ni kuwa iwapo wataitumia teknoljia hii kwa njia sahihi basi wataweza kufaidika sana hasa kielimu na katika upande wa pili iwapo teknolojia hii itatumika vibaya ndani ya nyumba si tu kuwa watoto watafeli katika masomo yao bali pia watakuwa na maadili maovu na pia kuharibu uhusiano na wazazi wao.
Wataalamu wa saikolojia wanaamini kuwa watoto wengi wanaelekea katika intaneti kutokana na mvuto wake, kujaza wakati wao wa mapumziko, kujaza pengo la nuksani katika maisha yao, kukosa utambulisho sahihi na pia kutokana na kuvurigika uhusiano baina yao na wazazi.
Wataalamu wa masuala ya jamii wanaamini kuwa, kuenea teknolojia ya habari na mawasiliano ni chanzo cha matatizo na upotofu wa kiutamaduni na kijamii duniani. Kuingia teknolojia ya mawasiliano manyumbani kuna maana ya kuingia kitu kipya na kisichojulikana ndani ya nyumba!
Iwapo teknolojia hii itatumiwa vibaya, basi kutatoweka fursa ya maingiliano ya kawaida baina ya jamaa katika familia na jambo hilo huibua hali ya kujitenga, upweke na ubinafsi miongoni mwa watu wanaoishi chini ya paa moja. Aidha intaneti huwafanya baadhi ya watu hasa watoto na mabarobaro kuwa ni wapokezi wa kilicho mbele yao pasina kuwa na uwezo wa kutosha wa kuchagua, kuchambua na kutafakari. Pamoja na hayo yote, tutake tusitake teknolojia sasa ni sehemu isiyotenganika na maisha ya kisasa. Leo watoto kuanzia umri wa hata chini ya miaka mitano wana hamu ya kuingia kwenye intaneti. Kwa hivyo sambamba na faida za teknolojia, hii kuna matatizo mengi ambayo huwakumba watu dhaifu kifikra katika jamii.
Leo wazazi na watoto hutumia wakati wao mwingi katika teknolojia za kidijitali ikiwemo intaneti na televisheni na hivyo hakupatikani fursa ya kutosha ya wazazi kuzungumza kwa karibu na watoto wao. Intaneti na vyombo vya habari vya kidijitali hupelekea kuongozeka ubinafsi na kujitenga mtu na jamii na hivyo kuporomoka zile thamani za maingiliano ya kijamii. Hivi sasa mabarobaro na vijana wengi wanatumia teknolojia mpya za habari na mawasiliano kupata elimu na maarifa. Hata watoto wadogo sawa na mabarobaro nao pia wanatumia teknolojia mpya kujitambulisha kuwa na marafiki kusoma na kuwasiliana na jamaa na marafiki. Kwa hivyo intaneti imegeuka na kuwa mwalimu katika maisha ya watoto na kwa kutegemea jinsi inavyotumika inaweza kuwa mwalimu mbaya au mzuri. Tatizo hili litakuwa sugu zaidi katika siku za usoni baada ya kuanza kutumika kizazi kipya cha intaneti iliyopewa jina la Web 4 ambayo haitawezekana kuifanyia filtering au kuzuia baadhi ya kurasa au tovuti za intaneti. Kwa mujibu wa inteneti hiyo ya mustakabali usio mbali wazazi na hata serikali haitaweza kudhibiti moja kwa moja kurasa zinazotembelewa hasa na watoto. Kwa msingi huo malezi yanatazamiwa kuondoka katika mkondo huu wa sasa na kuelekea upande wa kujilea au kujielimisa kupitia intaneti. Hapo hatari kubwa ni kuwa watoto wadogo, mabarobaro na vijana watakumbana na thamani nzuri na mbaya kwa pamoja na iwapo hakutakuwepo na muongozo sahihi basi wengine wataporomoka kimaadili na hali hiyo kuenea katika jamii.
Kwa hivyo kuna haja kwa wazazi kupata mafunzo kamili na ya kina kuhusu utumizi wa intaneti na teknolojia husika ili waweze kuwapa watoto ushauri na muongozo sahihi. Kinyume na hili hawatakuwa na uwezo wa kutoa ushauri kwa watoto wao. Wazazi wanapaswa kufahamu kuwa teknolojia ya habari na mawasiliano na hasa intaneti ni zaidi ya chombo cha kujipatia maarifa na kucheza. Kwa hakika intaneti sasa ni chombo kinachoweza kujenga au kusambaratisha utamaduni asili kwa hivyo kuna haja kwa walimu na wazazi kuinua kiwango chao cha ufahamu na ujuzi wa teknolojia za kisasa zinazotumiwa na watoto. Kwa mfano katika baadhi ya nchi hasa za Magharibi imebainika kuwa watoto walio kati ya umri wa miaka hadi minane hufuatilia kazi ambazo huwa wamekatazwa. Wakiwa kwenye intaneti huenda katika tovuti au mitandao ya kijamii wanakoweza kujuana na watu ambao ni hatari. Katika umri huu wazazi wanapaswa kuwaongoza watoto wao watembelee tovuti ambazo ni maalumu kwa watoto ili wasihadaiwe na watu wanaotaka kuwadhalilisha kijinsia. Watoto walio na umri wa kati ya miaka 9 hadi 12 huwa wameshaanza kutambua tafauti za kijinsia baina ya mwanaume na mwanamke na hivyo wazazi hapa pia wanapaswa kuchukua tahadhari ili watoto wao wasije wakatumbukia katika tovuti za ufuska

No comments:

Post a Comment